Papa Yohane Paulo II (kwaKilatini:Ioannes Paulus PP. II; kwaKiitalia:Giovanni Paolo II; kwaKipolandi:Jan Paweł II; kwaKiingereza:John Paul II;18 Mei1920 -2 Aprili2005) alikuwa Papa wa 264 kuanzia tarehe 16 Oktoba 1978 hadi kifo chake akidumu katika huduma hiyo kirefu kuliko Mapapa wengine wote, isipokuwa Mtume Petro na Papa Pius IX. AlitokeaWadowice,Krakow,Polandi.
Alimfuata Papa Yohane Paulo I akiwa Papa wa kwanza asiye Mwitalia tangu miaka 455 iliyopita, wakati wa Mholanzi Papa Adrian VI (1522 - 1523), tena Papa wa kwanza kutoka Polandi (na makabila yoyote ya Waslavi) katika historia ya Kanisa. Alifuatwa na Papa Benedikto XVI.
Jina lake la kuzaliwa lilikuwa Karol Józef Wojtyła (matamshi: ˈkarɔl ˈjuzɛf vɔiˈtɨwa).
Wengi wanamhesabu kati ya watu walioathiri zaidi karne ya 20, hasa kwa sababu tangu mwanzo wa Upapa wake alipambana na Ukomunisti uliotesa nchi yake asili na nyinginezo, akachangia kwa kiasi kikubwa kikomo chake na kusambaratika kwa Urusi.
Vilevile alilaumu ubepari wa nchi za magharibi na kudai haki katika jamii zote, akitetea hasa uhai wa binadamu na uhuru wa dini.
Upande wa dini, aliboresha uhusiano kati ya Kanisa Katoliki na madhehebu mengine ya Ukristo[11] pamoja na ule na dini mbalimbali, kuanzia Uyahudi, Ubudha, Uislamu.
Ziara zake 104 kati nchi 129 ulimwenguni kote, mbali na 146 nchini Italia na 317 katika parokia za Roma, zilikusanya mara nyingi umati mkubwa (hadi zaidi ya milioni 4 huko Manila, Ufilipino, mwishoni mwa siku ya kimataifa ya vijana), na kumfanya asafiri kuliko jumla ya mapapa wote waliomtangulia, akiwa mmojawapo kati ya viongozi wa dunia waliosafiri zaidi.
Papa Wojtyła alitangaza wenye heri 1,340 na watakatifu 483, ili kuwapa Wakristo wa leo vielelezo mbalimbali kwa maisha yao ili walenge utakatifu walioitiwa na Mungu. Idadi hiyo ni kubwa kuliko ile ya waliotangazwa na jumla ya Mapapa wote waliomtangulia walau katika karne tano za mwisho.
Alikuwa anaongea lugha mbalimbali, zikiwemo za Kipolandi, Kiitalia, Kifaransa, Kijerumani, Kiingereza, Kihispania, Kireno, Kiukraina, Kirusi, Kiserbokroatia, Kiesperanto, Kilatini na Kigiriki cha kale.
Yohane Paulo II alitangazwa na mwandamizi wake Papa Benedikto XVI kuwa mwenye heri tarehe 1 Mei 2011, halafu Papa Fransisko akamtangaza mtakatifu tarehe 27 Aprili 2014.
Sikukuu yake huadhimishwa kila mwaka tarehe 22 Oktoba[26], kulingana na siku ya kuanza rasmi huduma yake ya Kipapa kwa Misa iliyofanyika katika uwanja mbele ya Basilika la Mt. Petro,Vatikani.►Soma zaidi